BAKITA LAPONGEZWA KWA KUTOA MAFUNZO YA KISWAHILI KWA WAANDISHI WAENDESHA OFISI

13 Dec, 2025
BAKITA LAPONGEZWA KWA KUTOA MAFUNZO YA KISWAHILI KWA WAANDISHI WAENDESHA OFISI

Mwenyekiti wa Chama cha Waandishi Waendesha Ofisi (TAPSEA), Bi. Zuhura Songambele Maganga, amefungua rasmi mafunzo ya matumizi ya Kiswahili fasaha na sanifu kwa Waandishi Waendesha Ofisi (WWO) yaliyofanyika leo, tarehe 18 Novemba 2025, katika ukumbi wa hoteli ya Morena mkoani Morogoro.

Akizungumza wakati wa ufunguzi, Bi. Zuhura amepongeza hatua za Baraza la Kiswahili la Taifa (BAKITA) katika kuandaa mafunzo hayo, na kusisitiza umuhimu wa kutumia Kiswahili sahihi katika mawasiliano ya kiserikali ili kuongeza ufanisi, uwajibikaji na utoaji bora wa huduma kwa wananchi.

Amebainisha kuwa mafunzo hayo ni muhimu katika kuboresha utendaji kazi, kuongeza ubunifu, na kuimarisha nidhamu ya kazi, kwa kuwa Waandishi Waendesha Ofisi ni kiungo muhimu katika usimamizi wa taarifa na uratibu wa mawasiliano ndani ya taasisi za umma.
Aidha,Bi. Zuhura ametoa wito kwa Waandishi Waendesha Ofisi kudumisha mshikamano na kuziomba taasisi ambazo bado hazijawasilisha watumishi wao kwenye programu hiyo kufanya hivyo, akisisitiza kwamba mafunzo haya ni uwekezaji muhimu katika kuboresha utoaji wa huduma kwa umma.

Mafunzo haya ni sehemu ya programu endelevu iliyoanza tangu Agosti 2025, ambayo tayari imewanufaisha zaidi ya washiriki 537 kutoka taasisi mbalimbali za serikali. Washiriki wamehimizwa kuwa mabalozi wa Kiswahili fasaha na sanifu katika maeneo yao ya kazi.

Akihitimisha hotuba yake, Bi. Zuhura amewataka washiriki wote kutumia fursa hiyo kuwa wasikivu na kuhakikisha ujuzi watakaoupata unatumika kikamilifu katika majukumu yao ya kila siku.