Category Title
BAKITA YAPELEKA KISWAHILI NA UTAMADUNI MASHARIKI CREATIVE ECONOMY EXPO 2026
Baraza la Kiswahili la Taifa (BAKITA) limeshiriki Maonesho ya Mashariki Creative Economy Expo 2026, yanayofanyika kuanzia tarehe 18–21 Agosti 2026 katika ukumbi wa Mlimani City jijini Dar es Salaam.
Mashariki Expo 2026 ni jukwaa linalolenga kukuza uchumi wa ubunifu, kuimarisha ushirikiano, kubadilishana maarifa na kuunganisha wabunifu, taasisi, wawekezaji na wadau mbalimbali katika kukuza thamani ya kazi za ubunifu, zikiwamo fasihi na utamaduni
Katika tukio hili, BAKITA itakuwepo kutoa huduma mbalimbali zikiwa ni pamoja na kuonesha na kusambaza machapisho yake, kama vile Kamusi Kuu ya Kiswahili, Kamusi ya Shule za Msingi, Furahia Kiswahili Hatua ya Kwanza Toleo la Pili pamoja na machapisho mengine yanayolenga kukuza na kuendeleza lugha ya Kiswahili.
Aidha, Mwenyekiti wa Bodi ya BAKITA, Prof. Martin Mhando, ni miongoni mwa wawasilishaji wa mada katika tukio hilo, akichangia mijadala inayogusa maendeleo ya sekta ya ubunifu na fursa zinazotokana na kazi bunilizi na za kitamaduni.
Karibu Mlimani City!
Tembelea banda la BAKITA, pata huduma, jifunze zaidi kuhusu Kiswahili na machapisho yetu na tushirikiane katika kuendeleza Kiswahili na Utamaduni wa Afrika
